15/11/2025
π MKATE WA LEO KUTOKA KWA WACHUNGAJI: || ..............................
Yoshua 20:1-9.
Miji ya Kimbilio na Kimbilio la Neema.
β Je, unajua kwamba Mungu amekutayarishia mahali pa kukimbilia kwa ajili ya usalama wako pale unapotenda makosa?
πͺ UTANGULIZI NA MUKTADHA:
Mungu alikuwa amemwagiza Musa aweke miji mitatu upande wa mashariki na mitatu upande wa magharibi wa Mto wa Yordani kuwa ni miji ya makimbilio. Yoshua 20 inaonyesha utekelezaji wa maagizo haya. Miji ya makimbilio ambayo ilikuwa inakaliwa na Walawi, ilikuwa ni mahali palipowekwa kwa ajili ya wale waliokuwa na tuhuma za mauaji (Kutoka 21:12-13, Hesabu 35:9-34, Kumbukumbu 4:41-43, 19:1-13). Ndugu wa karibu wa marehemu alikuwa ana wajibu wa kulipiza kisasi kwa kumuua mkosaji. Mungu anamwagiza Yoshua kuchagua miji ya kimbilio ambamo mtu aliyemuua mwenzake bila kukusudia anaweza kukimbilia ili apate usalama mpaka mahak**a iamue. Na lango la mji lilikuwa linahusisha mahali ambapo palikuwa panaamua nani aruhusiwe kuingia na kutoka na kuweka ulinzi wa mji. Na pia Ζulikuwa na jengo lenye vyumba kadhaa ambapo wazee wa mji walipatumia k**a mahak**a na hata walipatumia kwa ajili ya biashara (Ruthu 4:1). Miji mitatu iko magharibi ya Yordani (Kedeshi, Shekemu na Hebroni) na mitatu iko mashariki (Bezeri, Ramothi na Golani). Mtu aliyesababisha kifo bila nia au bila kukusudia, alipaswa akimbilie mji huo, asimame kwenye lango na kueleza kesi yake. Atapokelewa na kuishi humo hadi kuhani mkuu afe; ndipo anaweza kurudi nyumbani bila kuadhibiwa. Miji hii inapatikana kwa wote, ikiwa ni pamoja na wageni. Hii inaonyesha haki na rehema katika utawala wa Mungu kwa watu wa mataifa yote.
π Soma Kwanza: Yoshua 20
Soma maagizo kuhusu miji ya makimbilio na jina la kila mji. Tafakari jinsi sheria hii inavyoonyesha haki, ulinzi na rehema na kupunguza umwagikaji wa damu au vifo vya kiholela na kuonyesha heshima kwa maisha ya mtu.
π MUUNDO WA MADA NA UCHAMBUZI WAKE:
πͺ’1. Agizo la Kuchagua Miji β Mst. 1β3 β Mungu anamwelekeza Yoshua ateue miji; watu wanaokimbilia huko wanapewa usalama mpaka kesi yao isikilizwe.
πͺ’2. Maagizo ya Utaratibu β Mst. 4β6 β Mwuaji wa bahati mbaya anatakiwa kuelezea kesi yake kwanza kwa wazee na baadaye kwa mkutano; anapewa ulinzi kwa kuhifadhiwa katika mahali palipoandaliwa hadi hukumu itakapotolewa. Ikithibitika aliua kwa makusudi anakabidhiwa kwa mlipiza kisasi ili apewe adhabu ya kifo kupitia ndugu wa karibu wa marehemu (Kumbukumbu 19:12). Na kwa yule ambaye aliua kwa bahati mbaya alitakiwa kubaki katika mji huu wa makimbilio hadi Kuhani Mkuu atakapokufa. Kifo cha kuhani mkuu kilikuwa kinaleta upatanisho, kwa sababu alipewa jukumu la kubeba hatia ya dhambi za watu (Kutoka 28:38 na Mambo ya Walawi 10:17). Hili jukumu la kifo cha makuhani wa agano la kale kubeba hatia za wenye dhambi liikuwa linaashiria jukumu la kafara ya Kuhani wa agano jipya Yesu Kristo kwa ajili ya ukombozi wa ulimwengu (1Petro 2:24 na Waebrania 9:11-15).
πͺ’3. Orodha ya Miji β Mst. 7β9 β Miji mitatu magharibi (Kedeshi, Shekemu, KiriathβArba/Hebron) na miji mitatu mashariki (Bezeri, Ramothi na Golani) inatajwa; sheria hii inatumika kwa waisraeli na wageni. Miji hii ya makimbilio pia ilikuwa miji ya Makuhani (Yoshua 21;13-38).
πͺ MUHTASARI WA MADA:
π΄1. Miji ya makimbilio ni ishara ya rehema ya Mungu: inatoa nafasi ya usalama na haki kwa wauaji wasio na nia mbaya.
π΄2. Hii inaonyesha kwamba Mungu anatofautisha kati ya kosa la kukusudia na la bahati mbaya.
π΄3. Pia inaonyesha jinsi Yesu alivyokuwa kimbilio letu β tunapomkimbilia tunapata msamaha na ulinzi dhidi ya adui.
π΄4. Sheria hii pia inatukumbusha kuanzisha mifumo ya haki katika jamii zetu na kuwatazama kwa huruma wale waliokosea bila kukusudia.
π₯ *MASWALI YA KUJADILI: JOSHUA 20:1-9*
β
1. Nia ya Mungu kuweka miji ya makimbilio ni kuepusha umwagaji damu usio na hatia na kutaka mtuhumiwa afikishwe kwenye vyombo vya kubaini makosa badala ya kila mmoja kujiamulia aonavyo. Unaona hali ya kuheshimu vyombo vya kutoa haki k**a mahak**a kwenye jamii unayoishi au kila mtu anajichukulia sheria mkononi? Je ni halali kumwadhibu mtu kwa kumdhania kuwa alikuwa anakusudia kutenda kosa?
β
2. Miji ya makimbilio ilimwakilisha Yesu aliye kimbilio la wenye dhambi. Je mtu aliyetenda dhambi ya kukusudia anaweza kusamehewa na Yesu? (Isaya 1:18). Miji ya makimbilio leo ni kituo cha polisi. Je unajisikia salama zaidi ukiwa mikononi mwa polisi? Baraza la Kanisa lina mamlaka ya kumsamehe mkosaji wakigundua alifanya kosa pasipo kukusudia?
β
3. Je amani huzalisha haki au haki ndiyo inayozalisha amani? Mahak**a zipo kwa ajili ya kudumisha amani au zipo kwa ajili ya kuwagombanisha watu? Je mtu aliyenyimwa haki anaweza kuwa na amani? Je kuna uwezekano mdhulumaji akamuona anayedai haki k**a anachochea vurugu na ukosefu wa amani?
β
4. Je, jamii yako ina mifumo gani ya haki na rehema kwa watu wanaokosea bila nia mbaya? Je wewe binafsi una utaratibu wenye huruma wa kuwatendea wale wanaokukosea kwa bahati mbaya?
β
5. Unajifunza nini kuhusu kumkimbilia Yesu k**a kimbilio lako wakati unapokosea? Je kuna uwezekano wa kufanya dhambi ambayo hukukusudia? Dhambi ambayo mtu anatenda wakati hajakusudiwa inahesabiwa kuwa ni dhambi? (Warumi 7:20).
π MASWALI YA TAFAKARI:
π1. Je unahitaji kujua kwamba unaweza kukimbilia wapi unapofanya makosa?
π2. Je, sheria hii inakutia changamoto kuanzisha mahali pa usalama na msamaha katika familia au jumuiya yako?
π§± MATUMIZI MAISHANI:
Waza njia za kuonyesha rehema kwa mtu aliyekukosea bila kukusudia. Toa kimbilio la maneno na matendo, ukikumbuka kwamba nawe unapokosea unahitaji rehema kutoka kwa Mungu kila siku. Msamehe mwenzi wa maisha, mtoto wako au mtu mwingine. Uwe tayari kumsamehe deni mtu anayeonekana kushindwa kulipa.
_Andiko la Kutia Moyo_
Naye atakaa katika mji huo, hadi hapo atakaposimama mbele ya mkutano kuhukumiwa, hadi kifo chake kuhani Mkuu mwenye kuwapo katika siku hizo; ndipo yule mwuaji atarudi , na kuuendea mji wake mwenyewe, hadi mji huo alioutoka hapo alipokimbia (Yoshua 20:6).
Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. (Zaburi 46:1).
_Neno la Baraka - Benediction_
Bwana akufungulie madirisha ya mbinguni na akumwagie baraka tele hata isiwepo nafasi ya kutosha na kikombe chako kijae kisukwe sukwe hata kumwagika. Bwana akuponye magonjwa yako, akupatie nguvu na afya njema na akuongezee siku za kuishi kwa furaha hapa duniani. Bwana aondoe dhoruba na akupatia upendo wa kweli katika ndoa yako na akujalie kuishi na amani na watu wote. Bwana abariki mashamba yako, biashara yako na kazi yoyote ya halali unayoifanya kwa bidii, ubunifu na bila kukata tamaa. Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe nawe sasa na hata milele.
_Tamko la Imani_
Hizi baraka ambazo zinatoka katika Neno la Mungu, ninazipokea kwa Imani na ninatanguliza shukrani kwa wema wa Bwana katika maisha yangu. Ninaamini hakika wema na fadhili zitanifuata siku zote za maisha yangu nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele (Zaburi 23:6).
π SALA YA MWISHO:
Mungu mwenye rehema nyingi, hakika wema wako na fadhili zako ni kuu sana na unastahili kuabudiwa. Nisaidie kujua kuwa usalama wangu unapatikana kwa kukimbilia kwa Jina la Yesu ambalo ni ngome imara na kila anayelikimbilia anakuwa salama. Kwa msaada wa Roho Mtakatifu niwezeshe kutambua kuwa wokovu wangu unapatikana kupitia kwa kifo cha msalabani cha Kuhani Mkuu Yesu Kristo na niwezeshe kumchagua Yeye kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yangu. Kwa sababu nimeutafuta ufalme wa mbinguni kwanza na haki yake, ninaomba unizidishie na mahitaji yangu mengine ya kimwili sawasawa na ahadi zako na wingi wa utajiri wako. Ninaomba kwa Imani kupitia kwa jina la Yesu, Amina.
π€π€π€ Watayarishaji wa Mwongozo huu wa Biblia: Pr. Stephen Letta, Pr. Lusekelo Mwakalindile, na Pr. Enos Mwakalindile, Dar es Salaam, Tanzania.
β‘οΈ Jiandae kwa Somo la Kesho: Sura ya 21 β Miji ya Walawi na Hakuna Ahadi iliyoanguka.